Monday, November 30, 2015

ELIMIKA KWA SHAIRI


3         KILA KIINGIACHO MJINI…

1.      Hivi kweli kila kiingiacho, mjini ni halali?

      Insi wakubali kila kinenwacho, ughaibuni ni halali!

      Maana waungama nacho, wakionapo runingani.

 

2.      Twakubali kwani tunamacho, hata hatuoni mbali!

      Ya ukweli na yasokificho, twabaini kila hali,

       Hii ni kweli kila kiingiacho, mjini ni halali?

 

3.      Kina dada wafanyacho, miilini wameridhi na kukubali!

      Wakwatuwa rangi zao na kubadili macho, ja shetani au si kweli?

      Watutumuwa maungo yao bila kificho, nasi twakubali

       Hii ni kweli kila kiingiacho, mjini ni halali?

 

4.      Kina kaka wakata mikato, ya kila sampuli

      Wafuasi kwa kila wakisikiacho, kwao ni makubuli

       Na wanafakhari watendacho, hata kama sicho kwa staili

       Au ndio kweli kila kiingiaho, mjini ni halali!

 

5.      Waduchu wafungua macho, wayaona nayo wayanakili,

      Wayadizaini, wayafuma na kuyaunda, mwisho, huwa makali kama pilipili,

      Waling’amua hawa kwa wakuu  wakifanyacho, alimradi kisulisuli!

      Ama kweli! Kila kiingiacho, mjini ni halali!

 

 

 

6.      Methali ni zetu kweli twazikubali!

      Kama fuata nyuki ili ule asali,

      Au chovyachovya hatimae, humaliza buyu la asali,

      Ama kilio huanza mfiwa, ndipo wa mbali,

      Na ile ya kivuli cha mvumo, hufunika aliye mbali,

       Pia ya mchele je! Mmoja, mapishi  ni mbali mbali,

       Ila nyengine si stahili, maana za umiza matumbo kweli,

        Kila kiingiacho mjini ni halali? Hii yanipa mushikeli.

 

SOMA SHAIRI UNUFAIKE


1.      TATA

1.      Ta! ta! Naanza kwa tata, kunena yanotokota,

      Tata hili lasokota, vichanga linaambata

      Wakuu nao wajuta, kwanini lawafuata

       Tata hili tata gani? Bado linatukung’uta.

 

2.      Juhudi zinatusuta, kulitokomeza tata,

      Kila leo tunateta, Bado limetufumbata,

      Twapiga ngumi ukuta, aah! Twajikunyata,

      Tata hili tata gani?  Bado linatukung’uta!  

 

3.      Sasa mwishoni nasita, na tena najiokota.

      Ta! Hili si la kugatwa, nanena tena nateta,

      Ogopa sije kudota! Utakuja kuufyata,

 

                        Tata hili tata gani?  Bado linatukung’uta.