Monday, July 25, 2016

SHAIRI -WINGU

WINGU
  1. Wingu bado limetanda, totoro metugubika,
            Kimbunga kinajiwinda, si dhani kama tavuka,
              Kiza nacho kimewanda, au ndo hayo masika?
              Wingu bado limetanda, mvua ndoto kunyeka.

  1. Kiza bado kimewanda, mvua imetoweka,
            Mipunga bado mikinda, vigumu kunawirika,
            Ndege nayo waiwinda, wataka kunufaika,
            Wingu bado limetanda, mvua ndoto kunyeka.

  1. Mipango nayo ni shinda, kumwagilia mashamba,
             Imekuwa ndugu donda, vipi litatuponyeka,
             Donda hili limevunda, harufu yake yanuka,
             Wingu bado limetanda, mvua ndoto kunyeka.

  1. Aridhi nayo ndandanda, kwa jembe ngumu limika,
            Wakulima yatushinda,  kuiburuga hakika,
            Mihindi tuloipanda, pole pole yanyauka,
            Wingu bado limetanda, mvua ndoto kunyeka.

  1. Wamechoka nao punda, nasi pia twahenyeka,
             Maji yamekuwa shinda, na ni machafu kunyweka,
             Wingu hili latutenda, lini tutaneemeka,

             Wingu bado limetanda, mvua ndoto kunyeka.

Tuesday, February 2, 2016

HATUA ZA KUFASIRI MATINI.


HATUA ZA KUFASIRI MATINI ZA AINA MBALI MBALI.
Mwansoko na wenzake (2006) Tafsiri ni zoezi la uhawilishaji (Transferring) wa mawazo katika maandishi kutoka lugha moja hadi lugha nyingine.

Merinyo, F. A (2014) akimnukuu Mshindo (2010:2) anasema kufasiri ni kufafanua maana ya matini moja na kutayarisha baadae matini nyengine inayowiyana nayo ambayo huitwa tafsiri na ambayo inawakilisha ujumbe ule ule uliomo katika matini ya awali kwa kutumia lugha nyengine.

Wataalamu mbali mbali wameainisha hatua kadhaa za kufuatwa katika mwenendo mzima wa kufasiri matini mbali mbali. Katika kujadili swali hili tutajadili hatua saba (7) kama zilivyoainshwa na Mwansoko na wenziwe  (2006). Hatua hizo ni kama ifuatavyo:

Hatua ya maandalizi, uchambuzi, uhawilishaji, rasimu ya kwanza, udurusu wa rasimu ya kwanza, kusomwa kwa rasimu na mtu mwengine na usawidi wa rasimu mwisho.


Hatua ya kwanza ni hatua ya maandalizi. Hatua hii inahusisha mambo matatu ambayo ni  Kupitia sehemu muhimu za matini chanzi, kwa mfano; istilahi, majina ya wahusika, majina ya kijiografia, maeneo au kauli zisizofasirika kirahisi. Kupata marejeleo ili kutafuta visawe vya kisemantiki. Kutafuta na kuandika visawe hivyo. Kadhalika hatua hii mfasiri huchunguza taarifa zinazohusu usuli wa matini chanzi. Hizi ni taarifa zinazohusu mwandishi wa matini, mazingira ya uandishi wa matini chanzi, malengo yake, utamaduni wa wazungumzaji wa matini chanzi na hadhira lengwa ya matini chanzi. Katika kuudurusu usuli wa matini chanzi mfasiri pia anapaswa kuzingatia sifa za kiisimu za matini anayotaka kuifasiri. Wakati huo huo mfasiri huandika pembeni (kwenye daftari maalumu) misamiati na istilahi muhimu maneno ya kitamaduni na sehemu ngumu katika matini chanzi ambazo zinahitaji uchunguzi na utafiti zaidi. 

Hatua ya pili ni uchambuzi. Katika hatua hii mfasiri huchunguza kwa makini maneno pamoja na maelezo muhimu ya matini chanzi aliyoyaandaa katika maandalizi ili aweze kuyatafutia visawe stahili katika lugha lengwa. Zoezi la uchambuzi hufanywa kwa kutumia marejeo mbali mbali, kama vile kamusi. Inashauriwa kuwa mfasiri awe na buku na notisi au faili kwa ajili ya kuandika na kuhifadhi maneno na maelezo muhimu na visawe vya matini chanzi. Visawe vilivyokubalika viorodheshwe vizuri ili iwe rahisi kurejelewa wakati wa kufasiri. Ikiwa matini chanzi ni kubwa sana mfasiri huwa hana budi ila ni kuigawa katika sehemu ndogo ndogo kama sura, aya na sentensi na kuitafasiri sehemu moja baada ya nyengine. Hata hivyo inashauriwa kwa mfasiri kwamba aya iwe ndio kizio cha msingi katika tendo la kufasiri.     


Hatua ya tatu baada ya maandalizi ni uhawilishaji (transferring/transference). Katika hatua hii mfasiri huhawilisha ile taarifa kutoka kwenye matini chanzi kwenda kwenye matini lengwa, hapa mfasiri anatakiwa kuzingatia sarufi ya lugha lengwa na lugha chanzi. mfano; “My new house is broken”-Yangu jipya nyumba ni vunjika. Tafsiri ya Kiswahili fasaha inapaswa kuwa “Nyumba yangu mpya imebomoka” Uhawilishaji maana yake ni kuhamisha maana, ujumbe nk. kutoka lugha chanzi kwenda lugha lengwa kwa kuzingatia sarufi ya lugha lengwa, lengo la matini au mwandishi, umbo la matini, mtindo nk.
Mbinu ya tafsiri ambayo inatumika katika hatua hii ya uhawilishaji ni tafsiri ya neno kwa neno.


Kadhalika hatua ya nne ni kusawidi rasimu ya kwanza (drafting). Uhawilishaji wa visawe kutoka lugha chanzi kwenda lugha lengwa unapokamilika kinachopatikana ni rasimu ya kwanza ya tafsiri. Rasimu ni kitendo cha kuandika matini au Makala yoyote kwa mara ya kwanza kwa mujibu wa utaratibu BAKIZA (2010). Mfasiri anapoanza kusawidi rasimu ya kwanza ya tafsiri yake atashuhudia kuwa anahitaji taarifa au ufafanuzi zaidi kuhusu uchambuzi aliokwishafanya mwanzo. Kwa hivyo atalazimika kufanya uchunguzi zaidi usuli wa matini na hata kupekuwa tena kamusi na marejeo mengine aliyotumia. Pia anapofanya uhawilishaji wa maana, mfasiri inafaa azingatie umbo la matini chanzi kuhakikisha kuwa linaakisiwa na matini lengwa. Mfano iwapo matini chanzi ni shairi la tathlitha (mistari mitatu) sura au umbo hilo halina budi kurudiwa katika matini lengwa. Akiwa nasawidi rasimu ya kwanza mfasiri inafaa afikirie hadhira anayoilenga pamoja na lengo la matini chanzi, kwani mambo haya huathiri mno usawidi wa tafsiri. Rasimu ya kwanza ya tafsiri inakuwa na dosari nyingi na kwa hiyo haifai kupelekwa kwa mteja au hadhira. Badala yake rasimu ya kwanza lazima ipitiwe tena na kurekebishwa au kudurusiwa.


Vile vile hatua ya tano ni kudurusu rasimu ya kwanza ili kuunda rasimu ya pili. Mfasiri hupata fursa ya kwanza ya kuitathimini na kuifanyia marekebisho tafsiri yake mwenyewe. Kazi ya kudurusu haipaswi kufanywa haraka. Wataalam wengine kama vile Larson (1984) anasema rasimu ya kwanza ni lazima iachwe kwa muda wa wiki moja. Udurusu unahusisha shughuli zifuatazo:
Kusahihisha makosa ya kisarufi, miundo isiyoeleweka vizuri.

Kunyoosha sehemu zenye tafsiri ya mzunguko na zenye matumizi potofu ya visawe. Mfano; “They rarely visit me these days – Siku hizi ni aghalabu-nadra sana wao kunitembelea.” Kurekebisha sehemu zenye muunganiko tenge au mbaya ambazo zinazuia mtiririko mzuri wa matini. Kuhakiki usahihi na kukubalika kwa maana zinazowasilishwa katika matini lengwa. Hapa tunaangalia kama kuna mambo yameongezwa, yamepunguzwa au yamepotoshwa/kubadilishwa. Kuhakiki kukubalika kwa lugha uliyotumia katika tafsiri yako kwa kuzingatia umbo na mada ya matini chanzi.
Kuona iwapo mada au ujumbe mkuu wa matini chanzi unajitokeza waziwazi katika matini lengwa.

Baada ya kuzingatia masahihisho hayo mfasiri atalazimika kutoa rasimu yake ya pili ambayo inashauriwa ampe msomaji mwengine ili aidurusu na kupendekeza masahihisho zaidi. Jambo hili litasababisha kwenda hatua nyengine inayofuata katika mwenendo wa kufasiri.

Kwa kuendelea hatua ya sita  ni kusomwa rasimu ya pili na mtu mwingine. Msomaji wa rasimu ya pili anaweza kuwa mfasiri au shabiki wa tafsiri, mhakiki au mhariri wa tafsiri, anaweza kuwa mpenzi wa tafsiri mbali mbali au mtu mwingine yeyote anayemwamini mfasiri. Katika hatua hii mfasiri anashauriwa atumie mbinu zifuatazo katika kumpata mtu mwengine ili kuisoma tena rasimu ya pili Kumpa bila kumjulisha kwamba ni tafsiri kumpa matini chanzi na matini lengwa ili alinganishe. Inapendekezwa kwamba mtu huyo asome kwa sauti ili uweze kubaini upungufu na iwapo atafikia pahala na kusita katika usomaji wake basi uwezekano mkubwa wa sehemu hizo za matini kuwa zina matatizo ya kiufasiri matatizo hayo yanaweza kuwa ni matumizi potofu ya viunganishi vya sentensi, upotoshaji wa maana za maneno, uendelezaji mbaya wa maumbo ya maneno au mikanganyiko katika matumizi ya mitindo. Hali hii ikitokea mtu aliyepewa kuidurusu rasimu ya pili atalazimika kuweka alama maalumu sehemu zenye matatizo na kisha kumuelekeza mfasiri azichunguze tena na kuzirekebisha.


Na mwisho ni hatua ya saba nayo ni kusawidi rasimu ya mwisho. Katika hatua hii mfasiri atafanyiakazi maoni na mapendekezo ya msomaji ambaye alimpa kazi yake. Matokeo ya kufanyiakazi maoni husababisha kupatikana kwa rasimu ya mwisho ambayo ndiyo humfikia mteja, hadhira, wachapaji na wengineo wanaolengwa iwafikie.

Hizi ndizo hatua zinazofaa kufuatwa katika mwenendo wa kufasiri matini za aina mbali mbali. Hata hivyo katika mwenendo halisi wa kufasiri inawezekana hatua hizi zisifuatwe katika mpangilio ulielezwa hapo juu. Hii ni kwa kuwa na ukweli kwamba wakati wa tendo la kufasiri mfasiri hulazimika daima kwenda mbele na nyuma kutoka katika matini chanzi mpaka kwenye matini lengwa. Pamoja na hayo ni muhimu kwa mfasiri kutambua kuwa kuna hatua zilizotajwa hapo juu katika mwenendo mzima wa kufasiri matini mbali mbali ambazo ni vyema kuzifuata kila inapowezekana.
 

MAREJEO.

Merinyo, F. A (2014). Tafsiri na Ukalimani (Utangulizi Muhimu katika Tafsiri

                               na Ukalimani). Mkuu-Rombo. Tanzania.

Cartford, J. C. (1965). A Linguistic Theory of Translation. London: OUP.
Larson, L. M. (1984). Meaning-based Translation. London: University Press

                               of America.
Mwansoko, H. J. M. na wenzake (2006). Kitangulizi cha Tafsiri: Nadharia na

                                                         Mbinu. Dar es Salaam: TUKI

BAKIZA (2010). Kamusi la Kiswahili Fasaha. OUP. Nairobi Kenya.
 

Tuesday, January 19, 2016

FASIHI NA UISLAMU


YALIYOMO

                  1.0       Utangulizi.

1.1              Miongoni mwa tabia na mwenendo mwema unaosabisha mja kuipata shahada mwisho wa maisha yake. 

1.2              Matendo mabaya na maovu yanayosababisha mja kukosa shahada wakati

wa kifo chake.

2.0      Hitimisho.  

1.0              Utangulizi

Uislamu ni mfumo kamili wa maisha na ndio dini inayokubalika na muumba wetu kama alivyosema katika Qur-ani kwamba dini anayoikubali M/Mungu ni uislmau. Kupitia hadithi ya Mtume iliyotoka kwa Abdur-Rahman Abdullah bin Umar bin Khattwab (r.a) anasema: Nimemsikia Mjumbe wa Allah (S.A.W) akisema “Uislamu umejengwa juu ya mambo matano: kushudia ya kuwa hakuna mola apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Allah na kuwa Muhammad ni Mjumbe wa Allah na kusimamisha swala na kutoa Zaka na kuhiji Nyumba Tukufu, na Saumu ya Ramadhan.” (Bukhar na Muslim). Tukiichunguza hadithi hii kwa makini inatuhakikishia kwamba “Kushudia ya kuwa hakuna mola apasaye kuabudiwa kwa haki ila ni Allah na kuwa Muhammad ni Mjumbe wa Allah. Ndio nguzo ya kwanza inayousimamisha uislamu na mja hana budi ili afanikiwe hapa duniani na akhera ni budi aishi kulingana na maamrisho aliyoyaamrisha Allah na Mtume wake, na ayaepuke yale yote yaliyokatazwa na Allah na Mjumbe wake.

Kwa mkabala wa kiislamu hakika hakuna tafauti ya dunia na dini ila kuna mambo ya kiislamu na yasiyokuwa ya kiislamu. Bila ya shaka jambo ambalo litaundwa kwa misingi ya kiislamu litakuwa la kiislamu kwa hivyo tamthilia ya “Shahada” imejaribu kwa kiasi kikubwa kuonesha matendo mbali mbali ambayo mtu akiyafanya huwa ni sababu mwisho wa maisha yake kuipata shahada na kuwa mja mwema. Kinyume chake imejaribu kuonesha matendo maovu ambayo yatamfanya mtu kujuta mwisho wa maisha yake na kuikosa shahada. Matendo hayo yameoneshwa kupitia wahusika walioicheza tamthilia hiyo kama vile Salami (Mume wa Mama Afrah na mwajiriwa wa Bw. Zuberi), Samira (Mke wa Zuberi), Zuberi (Mwajiri wa Salami), Kifimbo (Rafiki wa Zuberi na Salami) na wengineo ambao wamebeba dhima mbali za tamthilia hii.

 Katika tamthilia ya “Shahada” tunajifunza kwamba tabia njema ndio ufunguo wa kuipata shahada katika maisha ya muislamu. Kama Mtume alivyowahimiza waumini kujipamba na tabia njema.

 Kutoka kwa Abdalla bin Amr (r.a) anaeleza kuwa Mtume wa Allah amesema “Aliyekipenzi changu kuliko wote katika nyinyi (waislamu) ni yule aliyewazidi kwa tabia njema” (Bukhari). Katika Imani ya kiislamu kushuhudia kuwa Mtume Muhammad ni Mjumbe wa M/Mungu na kufuata aliyoyaelekeza kupitia suna yake ndio shahada ya pili.

Pia kutoka kwa Abu Hurairah (r.a) amesimulia kuwa Mtume (S.A.W) aliulizwa juu ya mambo yatayopelekea watu wengi kuingia peponi, akajibu Mtume “Uchaji mungu na tabia njema.” Kisha akaulizwa tena ni mambo yepi yatakayompelekea mtu kuingizwa motoni? Alijibu Mtume (s.a.w) “Mdomo na tupu (viungo vya siri)” (Tilmidhy).

Hivyo muumini wa kweli hana budi kujipamba na vipengele vya tabia njema vilivyoainishwa katika Qur-ani na Sunna ili iwe rahisi kuipata shahada mwisho wa maisha yake hapa ulimwenguni. 

 

1.1 Miongoni mwa tabia na mwenendo mwema unaosabisha mja kuipata shahada mwisho wa maisha yake. 

Kujielimisha kwa ajili ya Allah. Ni katika vipengele vya tabia njema ambayo mja humfanya kuipata shahada mwisho wa maisha yake. Kwa kupitia tamthilia ya “Shahada” Salami mwanzo kabisa wa tamthilia anatuonesha kuwa yeye ameshikamana na maisha ya kheri (kwamba ameshudia ya kuwa hakuna mola apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Allah na kuwa Muhammad ni Mjumbe wa Allah) na kupitia maisha hayo yanaashiria mwisho mwema wa maisha yake. Salami anatuonesha kuwa ni mtambuzi wa mambo katika maisha yake. Na bila ya shaka alijielimisha kwa ajili ya Allah. Hapa tunaona Salami alimsitiri muislamu mwenziwe alipopata ajali na kufariki dunia. Alishiriki kikamilifu katika kumuosha na hatimae kumzika. Bila ya elimu matendo haya asingeweza kuyatenda. Elimu ndio zana aliyotunukiwa mwanaadamu ili aitumie kutekeleza majukumu yake hapa ulimwenguni. Kama Qur-ani inavyosema. “Je wanaweza kuwa sawa wale wanaojua na wale wasiojua?” wanaotanabahi ni wale wenye akili tu.” (39:9) Na ni hakika sio sawa baina ya Salami na wale waliokimbia na gari baada ya kumgonga muislamu mwenzao na kusababisha kifo chake bila ya kujali.  

Kuwa na hekima. Hekima ni katika vipengele vya tabia njema vilivyoazizi anavyotakiwa avipiganie muumini ili awe na hadhi inayostahiki na ili aipate shahada mwisho wa maisha yake. Qur-an (2:269) “Allah humpa hekma amtakaye na aliyepewa hekma bila ya shaka amepewa kheri nyingi. Na hawakumbuki ila wenye akili.” Hiki ni kipengele chengine cha tabia njema kama kinavyooneshwa katika tamthilia ya “Shahada”. Na hapa tunaoneshwa kupitia muhusika Samira alipokuwa akimkumbusha Salami maovu yaliyofanywa na mumewe Zuberi kwa kusema “Si unajua alivyo kisirani, si unakumbuka jana alivyokuwa akikufanya. Yani hivi vitendo havipaendezewi  kabisa kibinaadamu. Na Nilivyoumia! Sana.” Salami alionesha wingi wa hekima kwa kutoa maneno ya hekima na msamaha na kutaka aombewe dua ili ajuwe anachokifanya kwani hayo aliyoyafanya kwa kutokujua kwa kusema “ Basi tumsamehe tu kwa sababu yeye hajui atendalo tunachotakiwa kumuombea dua na mungu amsaidie na sio vizuri tena kumuongelea” . 

Kadhalika Ikhalas ni katika vipengele vya tabia njema inayoweza kusababishia mtu kuipata shahada mwisho wa maisha yake. Ikhlasi ni kufanya kila jambo jema kwa ajili ya Allah tu. Yaani kutoa huduma na mali kwa watu wanaohitaji msaada bila ya kutarajia malipo yoyote kutoka kwao ila kutoka kwa Allah (s.w) Kwa Mfano kumlisha na kumvisha fukara, masikini au yatima bila ya kutarajia hata kupata shukurani kutoka kwake ila tu kwa kutegemea malipo kutoka kwa Allah. Qur-an (76:8-10) “Na huwalisha chakula masikini na yatima na wafungwa na hali ya kuwa wenyewe wanakipenda chakula hicho. Husema moyoni mwao wanapowapa chakula hicho tunakulisheni kwa ajili a kutaka radhi ya M/Mungu tu. Hatutaki kwenu malipo wala shukurani. Hakika sisi tunamuogopa mola wetu hiyo siku yenye shida na tabu” Hali hii inajitokeza pale ambapo Bibi kipofu na mwanawe walipokwenda kwa  Tajiri Zuberi kuomba msaada. Zuberi kwa kiburi na jeuri na hata kuwapiga alikataa kuwapa msaada walioutaka. Lakini Salami alionesha wingi wa ikhlas kwa kuwasaidia watu hawa bila ya kutarajia malipo kutoka kwao kwa kuwa alikiri kuwa hapana mola apasae kuabudiwa kwa haki ila Allah na Mtume (S.W.A) ni mjumbe wake.   

 

Kujiepusha na riya na kujiona. Pia ni kipengele cha tabia njema ambacho humfanya mja kuipata shahada mwisho wa maisha. Riya ni kinyume cha ikhlasi. Kufanya riya ni kufanya jambo jema ili watu wakuone wakusifu wakupe shukurani. Mtu anaefanya riya hafanyi wema kwa kutarajia malipo kutoka kwa Allah (s.w) bali hufanya kwa kutarajia malipo ya hapa duniani tu iwe ni mali, sifa au shukurani. Haya tunayapata pale Salami alipomlipia Kifimbo alipokuwa akidaiwa na kushurutishwa kulilipa deni wanaomdai bila ya kuwa na uwezo wa kulilipa. Salami aliyafanya haya bila ya kutaraji sifa au shukurani ila ni kutaraji malipo kutoka kwa Allah. Qur-ani (11:15-16) M/Mungu anasema “Wanaotaka maisha ya dunia na makombo yake, tutawapa huku duniani (ujira wa) vitendo vyao kamili humu wao hawatapunjwa. Hao ndio ambao hawatakuwa na kitu katika akhera ila moto na wataruka patupu walioyafanya katika dunia hii na yatakuwa bure waliyokuwa wakiyatenda.

 

Kujiepusha na zinaa na tabia za kizinifu. Hiki pia ni kipengele cha tabia njema ambacho bila ya shaka mja akidumu nacho huwa ni sababu kwake kuipata shahada. Waumini wa kweli waliofuzu hujihifadhi na zinaa au kujiepusha kufanya jimai nje ya mipaka iliyowekwa na Allah (s.w). Muumini wa kweli aliyekiri kuwa hapana mola apasae kuabudiwa kwa haki ila Allah na Mtume ni Mjumbe wake hutekeleza bila ya kusita ile amri ya Allah (s.w) ya katazo la “ Wala usiikaribie zinaa kwa hakika huo ni uchafu na ni njia mbaya kabisa . (17:32). Katazo hili alilitekeleza Salami katika tamthilia ya “Shahada” na nikutokana na hilo ndio ikawa chanzo cha kifo chake na alikufa akiitoa shahada kwamba ameshuhudia kuwa hapana mola apasae kuabudiwa kwa haki ila Allah na Mtume ni Mjumbe wake. Mbali na vishawishi vya Samira mke wa mwajiri wake kumlazimisha kutembea nae lakini Salami alikuwa na msimamo na kukataa katakata. Matendo haya mema na mwenendo wa muhusika Salami ndio yaliyosababisha Salami kufa kifo chema cha kuitamka shahada. Hivyo ni kweli kwamba kuipata shahada kunategemea na maisha anayoishi mja.   

 

1.2 Matendo mabaya na maovu yanayosababisha mja kukosa shahada wakati wa kifo chake.

Kinyume chake kwa matendo maovu na mwenendo mbaya ni sababu kubwa kwa mja kushindwa kuitamka shahada mwisho wa maisha yake hapa ulimwenguni. Na ushahidi kamili tunaupata mwisho Zuberi alijutia yote aliyoyafanya na kushidwa kuipata shahada wakati wa mauti yake yalipomfikia. Miongoni mwa matendo hayo maovu yaliyomkosesha shahada Zuberi na wenzake kama Kifimbo ni kama yafutayo:-

Dharau. Hiki ni kipengele kimoja wapo cha mwenendo mbaya ambacho huweza kumuepusha mja kuitamka shahada mwisho wa maisha yake. Mwenye kuwadharau wengine hujihisi kuwa yeye bora kuliko mwengine. Hili ni kosa kubwa kwani anayejua aliye mbora ni Allah (s.w) Pekee kama tunavyojifunza katia Qur-an. “Enyi watu! Kwa hakika tumekuumbeni (nyote) kutoka kwa (yule) mwanaume ; Adam na yule mwanamke (mmoja; Hawwa). Na tumekufanye mataifa na makabila (mbali mbali) ili mjuane. Hakika ahishimiwaye sana miongoni mwenu mbele ya M/Mungu ni yule amchaye Mungu Zaidi katika nyinyi…” (49:13). Tajiri Zuberi alimdharau sana Salami, alimuona mjinga sana hata kumwita “Bwege nazi mkubwa”, “Kelbu mkubwa”, “Mshenzi wewe” “Shuwaini”,  Kenge maji”, “Punda”. Haya na mengine ndio yaliyomsababisha Tajiri Zuberi kuikosa shahada wakati wa kifo chake.

Tabia ya matusi na maneno machafu. Pia ni mwenendo mbaya ambao bila ya shaka huweza kumzuia mja wakati wa kutoka roho yake kuitamka shahada. Tajiri Zuberi alikuwa na matusi na maneno machafu katika kinywa chake kwa lengo la kumdhalilisha Salami. Kwa waislamu kuna katazo kubwa juu ya hilo. Tumekatazwa kutukanana na hata kuitana majina tusiyoyapenda kwa kejeli. M/mungu katika Qur-an anasema “…Wala msitukanane kwa kabila wala msiitane majina mabaya (ya kejeli). Jina baya kabisa kuitwa mtu ni “Fasiq” baada ya kuwa yeye ni muislamu. Na wasio tubu basi hao ndio madhalimu. (49:11). Tukirejea mafundisho ya Mtume tunayapata kupitia hadithi kutoka kwa Abu Hurairah (r.a) amesimulia kuwa Mtume (S.A.W) aliulizwa juu ya mambo yatayopelekea watu wengi kuingia peponi, akajibu Mtume “Uchaji mungu na tabia njema.” Kisha akaulizwa tena ni mambo yepi yatakayompelekea mtu kuingizwa motoni? Alijibu Mtume “Mdomo na tupu (viungo vya siri)” (Tilmidhy). Kwa hiyo jambo moja kubwa alilokuwa nalo Tajiri Zuberi ni Mdomo mchafu na huu ndio uliomkosesha kuitamka shahada wakati wa kifo chake.

Kadhalika kutokuwa na huruma. Ni miongoni mwa mwenendo mbaya ambao humzuia mja kuikosa shahada mwisho wa maisha yake. Tajiri Zuberi alijipamba na mwenendo huu ovu wa kutokuwa na huruma. Aliwashambulia masikini waliokuwa na mahitaji kwa jeuri na kiburi na mwisho kuwafukuza bila ya huruma kwake na haya ndio yalikuwa maneno yake walipokuwa wakijibizana na masikini waliokuja kutaka msaada. “ Kwanza nani aliyewatuma mje hapa? Hivi mimi naweza kuzaa mjusi kama wewe! Nakuuliza naweza kuzaa mjusi kama wewe? Na wewe mama kipofu umepita majumba yote huko hukuona pakuingia isipokuwa huku eh! Nikusaidie nini? Toka hebu kwenda huko na wee mama nenda huko pumbavu! Kwendeni!”

Muunini wa kweli hana budi kujipamba na tabia ya kuhurumia viumbe  wenzake. Amuonee huruma kila mwenye shida na ajitahidi kumsaidia inavyowezekana. Katika kuonesha umuhimu wa kipengele hiki katika uislamu Mtume (s.a.w) amesema “Ambaye hahurumii watu, pia Allah (s.w) hatamhurumia” (Bukhari). Huruma hudhihiri katika kuwasaidia wenye shida na matatizo kwa mali na kauli kama Qur-ani inavyotufunza “ Hamtaweza kufikia wema mpaka mtoe katika vitu mnavyovipenda na chochote mnachokitoa, basi hakika Allah anakijua”. (3:92). Tabia hii mbaya ya kutokuwa na huruma kwa wenye shida ndio moja miongoni mwa nyingi zilizomponza Tajiri Zuberi kuikosa shahada wakati wa kifo chake.

 

Unafiki ni miongoni mwa tabia mbaya na ovu kwa muumini. Mnafiki ni yule anaekubali uislamu mdomoni (kwa kauli tu) lakini moyoni mwake na katika matendo yake anaukanusha. Kupitia Qur-an (2:8-9). “ Na katika watu wako wasemao tumemuamini M/Mungu na siku ya mwisho hali ya kuwa wao si wenye kuamini. Wanataka kumdanganya Allah na wale walioamini, lakini hawadanganyi ila nafsi zao, nao hawatambui”. Kifimbo kaonesha unafiki pale anapokuja kwa Salami muislamu mwenziwe ni mtu mwema wakati huo huo akenda kazini kwake anamchongea kwa mwajiri  wake. Na akirudi tena kwa Salami humchonganisha yeye na mkewe, na hatima yake mke wa Salami kuomba talaka kwa mumewe kwa unafiki wa Kifimbo kusema kuwa Salami ana mke mwengine. Matendo haya ya Kifimbo ni ya kinafiki na ni matendo maovu ambayo yanaweza kuwa sababu kwa mja kuikosa shahada mwisho wa maisha yake.

Kiburi na majivuno. Kiburi, majivuno na majigambo ni katika tabia mbaya iliyokemewa vikali katika Qur-an kama ifuatavyo (31:18). “Wala usiwatazame (watu) kwa upande mmoja wa uso, wala usiende katika ardhi kwa maringo, hakika Allah hampendi kila ajivunae ajifaharishaye” Zuberi anajiona kuwa ni bora kwa Salami na ni wajuu na wa maana zaidi kuliko Salami. Kiburi hicho na kujiona kulisababishwa na neema (utajiri) aliotunukiwa na mola wake. Tabia hii ovu ndio iliyokuwa sababu kwa tajiri Zuberi kujuta na kuikosa shahada wakati kifo kilipomfikia.

Kuikimbilia zinaa na tabia za kizinifu. Ni miongoni mwa tabia mbaya ambayo ni moja kati ya zile zinazoweza kumzuia mja kuipata shahada mwisho wa maisha yake. Katika tamthilia ya “Shahada” tumeoneshwa Samira (mke wa tajiri Zuberi) ni mwenye kuikimbilia zinaa na ni mwenye tabia za kizinifu. Samira alifanya kila analoweza kumrubuni Salami atekeleze matamanio yake anayotaka. Alimpa pesa sio kwa kumsaidia bali kwa lengo la kumhonga. Hatima yake alimfungia milango kwa kumlazimisha afanye nae zinaa japo kwa mara moja tu. Na jambo hili ndio sababu kwa mumewe kumteka Salami na kumuadhibu. Na pia ndio sababu kupoteza maisha yake bila ya kuipata shahada. Mwenendo huu na tabia hii ya uzinifu sio tabia njema kwa muumini aliyeshuhudia  kuwa hakuna mola apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Allah na kuwa Muhammad ni Mjumbe wa Allah.  


2.0 Hitimisho

Kupitia tamthilia ya “Shahada” ni dhahiri kwamba kuipata shahada mwisho wa maisha ya mja duniani kunategemea na jinsi anavyoendesha mja maisha yake. Haya yanathibitika kupitia muhusika Salami ambapo maisha yake yote aliishi kwa kujipamba na tabia njema na kutennda yaliyo mema kama vile kujielimisha kwa ajili ya Allah kwa kutenda matendo mema kwa ujuzi na elimu sahihi, kuwa na hekima, kuwa na ikhlasi, kujiepusha n aria, na kujikinga na zinaa. Na kinyume chake kuikosa shahada kunategemea na mwenendo wake hapa ulimwenguni. Haya tunaoneshwa na Tajiri Zuberi katika tamthilia ya “Shahada” pale alipojipamba na tabia mbaya na mwenendo mbaya kama vile; kuwa nadharau, kuwa na tabia ya matusi na maneno machafu, kutokuwa na huruma, na kuwa na kiburi na majivuno ya kupindukia. Haya na mengineyo ndio sababu kwake kuikosa shahada mwisho wa maisha yake.   


MAREJEO

Al-farsy, A. S (1993).Qur-an Takatifu, The Islamic Foundation. Nairobi Kenya.

An-Nawawi, Y. S (2009). Matnu Arbain Nawiyyah na Tafsiri yake. Ibn Hazm Media Center. Dar-es-salaam. Tanzania.


IPC. (2003). Nguzo za Uislamu, Darasa la Watu Wazima Juzuu ya 2. Islamic Propagation Centre DSM. Tanzania.