Monday, December 21, 2015

SWALA NI AMALI ADHIMA


Swala  amali adhima.

 

1.     Swala tano ni lazima,         kwa mumini isilama,

          Lazima afanye hima,          kuziswali kiheshima,

          Nathawabu atachuma,        kwa mzima na kilema,

          Isilamu hima hima,            swala amali adhima.

2.     Dada haya jisukuma,         Jumamosi na Ijuma,

Adhana ikilalama,              itika nawe kusoma,

Kaswali usiwe nyuma,       ukazivune neema

          Isilamu hima hima,            swala amali adhima.

3.     Kwenye siku hurindima,   tano huwa kusimama,

Adhuhuri nikisema,            ni rakaa nne nzima,

Tekeleza isilama,              swala ni nguzo nzima

          Isilamu hima hima,           swala amali adhima.

4.     Laasiri si hekima,             kuiacha ikikoma,

Magharibi kwa heshima,  kaswali ni jambo jema,

Tenda ukiwa mzima,        Pandu na wewe Salama,

          Isilamu hima hima,           swala amali adhima.

5.      Isha, fajir simama,           uondoshe yako dhima,

Safisha yako khatima,      uwe salama kiyama

Uiepuke nakama,              kwenye moto jahanama,

          Isilamu hima hima,           swala amali adhima