Monday, December 29, 2014

MAENDELEO YA FASIHI ANDISHI ZANZIBAR( RIWAYA, TAMTHILIA, USHAIRI, HADITHI FUPI)



Tafauti ya maendeleo ya fasihi andishi ya Zanzibar kabla ya uruhu na baada ya uhuru katika vipengele vya Hadithi fupi, Riwaya, Ushairi na Tamthilia ni kama ifuatavyo. Tutajadili kwanza Riwaya, pili Ushairi tatu hadithi fupi na mwisho ni tamthilia. 
Riwaya.  
Kwa mujibu wa Wamitila (2003) anasema riwaya ni kazi ya kinathari au kibunilizi ambao huwa na urefu wa kutosha, msuko uliojengeka vizuri, wahusika wengi walioendelezwa kwa kina, yenye kuchua muda mwingi katika maandalizi na kuhusisha mandhari maalumu.
Mkwera  (1978) anasema kuwa riwaya ni hadithi iliyo ndefu kuweza kutosha kufanya kitabu kimoja au zaidi.
Muhando na Balisidya. (1976) wanaeleza riwaya ni kazi ya kubuni, ni hadthi ambayo hutungwa kufuatana na uwezo wa fanani kuibusha mambo kutokana na mazoea au mazingira yake. Wanaendelea kusema kuwa riwaya yaweza kuanzia maneno 35000 hivi na kuendelea.    
Ukubwa wa riwaya, unaweza kuwa wa kurasa zozote zile kwani si idadi ya maneno au kurasa tu ambavyo vitatufanya tuiite hadithi fulani kuwa ni riwaya na nyingine kuwa hadithi fupi, zipo riwaya kana Nyota ya rehema (1981) kuli (1979)

Tukianza kuzungumzia historia ya riwaya ya Kiswahili ni muhimu kuihusisha sana na fasihi simulizi. Uhusiano huu sio wa kimuundo, ingawa muundo wa masimulizi ulichangia kwa kiasi fulani katika riwarya nyingi za mwanzo, lakini zaidi ni uhusiano uliotokana na uandikaji wa hadithi za Kiswahili. Edward Steere alipokusanya na kuhariri hadithi alizozipata kutoka kwa wakazi hadithi alizozipata tutoka kwa wakazi wa Zanzibar unaweza kuwa ndio wakati wa kwanza kuangalia histori ya riwaya yetu ya Kiswahili (Mlacha na Madumulla, 1991:11).
Kwa mujibu wa Mulokozi anasema kuwa chimbuko la riwaya lipo katika mambo makuu mawili
Moja ni fani za kijadi za fasihi na pili ni mazingira ya kijamii

Fani za kijadi kama vile:-
Ngano-hadithi za kubuni zinazohusu wanyama, watunzi wengi wameathiriwa na ngano kw wasababu wanachota visa, mbinu za kifani , dhamira katika ngano (zinaonekana kwamba ni za kingano zaidi)

Visasili-masimulizi ya kubuni ambayo yanaeleza juu ya maisha, asili, ya vitu na hatima yake. Kwa kawaida visasili huaminiwa kuwa ni hadithi za kweli

 Visakale ni hadithi za kale kuhusu mashujaa wa taifa, kabila au dini. Mara nyingi visa kale huchanganywa na historia na masimulizi ya kubuni na hadithi hizi hupatikana katika kila kabila au kila lugha. Baadhi ya visa kale vya Kiswahili ni masimulizi kuhusu miji ya pwani na Zanzibar. Mfano mzuri ni hadithi ya Abdallah Bin Hemed bin Ali Ajjemy (1972) 

Hekaya-ni hadithi za kusisimua kuhusu masaibu na matukio ya ajabu yasiyo ya kawaida, mara nyingi masaibu yanasababishwa na mapenzi, huwa ni ndefu kuliko hadithi nyingine lakini si ndefu kuliko riwaya.

Tendi-ni hadithi ya kishairi kuhusu mashujaa wa kihistoria na wakubuni wa jamii au taifa
 Masimulizi ya wasafiri. Hizi ni habari zinazosimulia masaibu ya wasafiri katika nchi mbali mbali. Hizi nazo zilisaidia kupatikana kwa riwaya. Mfano Alfa-lela-ulela.

Katika karne ya 16 fani nyingi ziliendelea. Na mojawapo ya sababu ya kuendelea kwa riwaya ilikuwa ni:
Ukuaji mkubwa wa shughuli za kiuchumi huko Ulaya baada mapinduzi ya kiviwanda

Mageuzi ya kijamii na kisiasa yaliyofungamana na mabadiliko ya kiuchumi

Ugunduzi wa teknolojia ya upigaji chapa

Maendeleo ya riwaya kabla ya uhuru Zanzibar.

Tukianza kuzungumzia historia ya riwaya ya Kiswahili za Zanzibar ni muhimu kuhihusisha sana na fasihi simulizi. Uhusiano huu sio wa kimuundo, ingawa muundo wa masimulizi ulichangia kwa kiasi fulani katika riwarya nyingi za mwanzo, lakini zaidi ni uhusiano uliotokana na uandikaji wa hadithi za Kiswahili. Edward Steere alipokusanya na kuhariri hadithi alizozipata kutoka kwa wakazi wa Zanzibar unaweza kuwa ndio wakati wa kwanza kuangalia histori ya riwaya yetu ya Kiswahili (Mlacha na Madumulla, 1991:11). Kwa hivyo tukiichambua nukuu hiyo tunaweza kusema kuwa historia ya riwaya za Zanzibar na maendeleo yake ilianzia karne ya 18 mara tu Bw. Edward Steere alipokusanya na kuhariri hadithi alizozipata kutoka kwa wakazi wa Zanzibar.
Kabla ya ukoloni sehemu kubwa ya fasihi andishi ya kimasimulizi ilikuwa ni tendi. Baadhi ya tendi hizo ni kama vile kisa cha Anzaruni au Siri lAsirari Binti Lemba:1663) Kadhi Kassim bin Jaafar Hemed Abdalla karne ya kumi na 9 zilitumia mbinu za kiriwaya kwa mfano ubunifu wa vituko, msuko na matukio ambazo ziliandaa mazingira ya kisanaa yaliyochangia kuzuka kwa riwaya.
Jambo jengine lililosaidia kuchipuza kwa riwaya Zanzibar ni tafsiri. Tafsiri za mwanzo katika lugha ya Kiswahili zilikuwa za kidini kwa mfano tafsiri ya kwanza iliyofahamika ni Sayyid Aidarus Bin Athuman karne 17. Kaswida ya Hamziyah 1652. Pia vilitafsiriwa vitabu vya hadithi kutoka lugha ya kiarabu kwa Kiswahili Mfano Hekaya Abunuasi na Alif-Lela-Ulela.

Kuundwa kwa kamati ya lugha ya Afrika mashariki mnamo mwaka 1929, kazi ya Kamati hii ilikuwa na nafasi kubwa sana katika kuendeleza lugha ya Kiswahili na fasihi ya Kiswahili. Na bila ya shaka iliendeleza riwaya za Zanzibar. Kamati pia iliandaa mashindano ya uandishi wa kazi za fasihi. Hali hii ilisababisha kutokea kwa waandishi wapya wa riwaya. Mfano wa mwandishi mashuhuri wa riwaya Muhammed Said Abdulla (BWANA MSA) na vitabu vyake kama vile Mzimu wa Watu wa Kale.(1958), Kisima cha Giningi (1958). Mwandishi mwengine wa riwaya za Zanzibar zilizoandikwa kabla ya uhuru ni mwandishi Muhammed, M. S na kitabu chake cha Kurwa na Doto (1960) katika kipindi hiki waandishi hasa wamezingatia namna jamii ilivyokuwa kabla ya uhuru Mfano: Mzimu wa watu wa kale kilikuwa na maudhui ya athari ya dhulma na upepelezi, Kurwa na Doto thamani ya utamaduni katika jamii mila na utamaduni. Na Kisima cha Giningi ni uongozi mbaya na ushirikina.
Baada ya uhuru riwaya za kiswahi zikiwemo za Zanzibar zilipevuka na kutanuka zaidi na hii ilikuwa kwenye miaka ya 1970-1975 kadhalika zilijitokeza riwaya za mikondo mbali mbali mambo makuu yaliyoipambanua riwaya ya Kiswahili ni
Moja kutokea kwa watunzi wapya vijana ambao wameipa uhai mpya riwaya Mfano Said Ahmed Muhamed, Shafi Adam Shafi Muhamed S. Abdulla.
Pili kuongezeka kwa riwaya pendwa ambako kuliambana na kutokeza kwa wachapishaji ambao walichapisha riwaya zao wenyewe.
Tatu kujitokeza kwa riwaya inayoihakiki jamii kwa undani ambazo wengine waliziita riwaya za uhalisia. Baadhi ya watunzi mashuhuri ni Shafi Adam Shafi na Kasri ya Mwinyi Fuadi(1978) na Kuli (1979), S, A Muhamed na Tata za Asumini (1990).
Nne kuzuka kwa riwaya za kihistoria mfano wa riwaya hizo ni Vutan’kuvute ya mwandishi Shafi Adam Shafi (1999).
tano kuanzishwa kwa taaluma ya uhakiki wa fasihi ya Kiswahili. Taaluma hiyo ilianza kufundishwa baada ya kuanzishwa kwa idara ya Kiswahili katika Chuo Kikuu cha Dar-es-salaam mnamo mwaka 1968-1970. Taaluma hii ilienezwa hadi mashuleni. Mulokozi, M.M(1996).
Ushairi.
Ushairi kwa mujibu wa Massamba D.P.B (2003) akimnukuu Shaaban Robert anasema ushairi ni Sanaa ya vina inayopambanuliwa kama nyimbo, mashairi na tenzi Zaidi ya kuwa na Sanaa ya vina ushairi una ufasaha wa maneno machache au muhtasari.
Mnyampala (1970)  anasema kuwa ushairi ni msingi wa maneno ya hekma tangu kale ndicho kitu kilichobora sana maongozo ya dunia kwa kutumia maneno ya mkato na lugha nzito yenye kunata iliyopangwa kwa urari wa mizani na vina maalum.
Amri Abeid (1954:1) anasema kuwa ushairi au utenzi ni wimbo hivyo kama shairi haliimbiki halina maana.  
Chimbuko la ushairi. Katika kipengele hiki kuna nadharia nyingi zinazoeleza juu ya chimbuko la ushairi wa Kiswahili.
Kuna nadharia inayosema kwamba ushairi wa Kiswahili chimbuko lake ni ujio wa waarabu, na nadharia nyengine ni ile ya ushairi kuwa ni zao la jamii ya waswahili wenyewe.
Nadharia ya pili ni ile ya ushairi chimbuko lake ni zao la waswahili wenyewe. Katika nadharia hii tunaweza kungundua kuwa ushairi hapo kale ulikuwepo hata kabla ya ujio wa wakoloni na ndio kipindi cha ushairi kabla ya uhuru. Nadharia hii imejadiliwa na wataalamu mbali mbali wakiwemo Shaban Robert, Jumanne Mayoka (1993) na F.E.M.K Senkoro, Mulokozi na Sengo. Tukianzia na Jumanne Mayoka (1993), yeye anasema kuwa ushairi umetokana na jamii ya wanaadamu wenyewe na umesheheneza ukwasi mkubwa wa lugha ambayo imekuwa ikitumika katika hatua zote za kisiasa, kiuchumi, na kiutamaduni katika historia ambayo mwanaadamu amepita. Kwa mfano kuwa msamiati uliotumika tangu enzi za kuishi mapangoni, enzi za uwindaji, ujima, utumwa, vita vya makabila au uvamizi wa wageni, ukoloni na harakati za kupambana na ukoloni hadi uhuru na maendeleo yake.
Senkoro (1988) anasema kuwa ushairi uliibuka pale lugha ilipoanza katika kipindi cha uhayawani (Kipindi ambacho mwanaadamu alipoanza kupambana na mazingira yake) kwenda katika kipindi cha urazini (maana)ili kumuezesha mwanaadamu na mazingira yake. Kwa Mfano zana za kazi zilizotumika ziliwafanya waimbe kwa kufuata mdundo wa zana hizo.
Tukiziangalia nadharia hizi mbali zinatuelekeza kuwa Zanzibar nayo ni miongoni mwa sehemu za pwani ya Afrika Mashariki ambako ndiko kunakopatika ushairi wa Kiswahili. Hivyo kwa namna yeyote ile imepitia historia hiyo na mabadiliko yake. Katika kulibainisha hili kuhusu hoja ya ushairi ni zao la waswahili wenyewe hata wazanzibari kuna nyimbo zilitumika katika kuwabembelezea watoto mfano wa nyimbo hiyo inasema:-
Owa mtoto owa, owa mtoto owa
Silia mwanangu silie, ukaniliza na mie
Machozi yako yaweke, nikifa unililie
Jipigepige makonde, watu wakushikilie

Kinoleo cha maboga, kutia nazi kunoga
Mkono wataka kula, maungo yaona woga

Kile kidau kijacho, hakikosi mna changu
Mna mkufu mpambe, kadiri ya shingo yangu
Aupata siuvai, wala simpi mwenzangu
Nampelekea mama, msiri wa mambo yangu

Owa owa mtoto owa, owa owa mwanangu owa
Kilelema kilelema, kitawi cha mlelema
Ukakichuma cha juu, cha chini kitakulema
Mti mshindao nyani, ujuwe una kilema…..
Wimbo huu hadi hii leo wanajamii wa Zanzibar wanaendelea kuutumia kwa shughuli ile ile ya malezi kwa watoto ambayo wazee wao waliitumia kuwalelea watoto wao.
Tukiangalia katika nadharia ya kwanza kuwa ushairi ulitokana na ujio wa waarabu. Hoja hii inatufungua macho kwamba ushairi inawezekana kwamba ulikuja enedelezwa baada ya ujio wa wageni. Kwa muktadha huu basi tunasema kuwa Zanzibar ni miongoni mwa maeneo yaliyowahi tawaliwa na waarabu kutoka Oman. Hoja hii imeungwa mkono na wataalamu mbali mbali kama vile Lyndon Harries (1962) katika kitabu chake kiitwacho Swahili Poetry anatoa ushahidi kuwa ushairi wa Kiswahili ulitokana na uislamu. Yeye anasema kuwa ushairi ulianzia kwenye upwa wa kaskazini mwa Kenya hususan Lamu. Utungo wa kwanza wa ushairi andishi wa Kiswahili ni Tambuka , Mwengo bin Athman (1728),waandishi wengine waliotunga tenzi miaka ya baadae baada ya hiyo ni mwandishi Chum Haji na utenzi wake uitwao Utenzi wa vita vya Uhudi  (1962).
Ushairi ulipita katika hatua mbali mbali katika maendeleo yake katika kipindi hiki baada ya ujio wa wageni inasemakana ilikuwa ni kipindi cha Utasa kama asemavyo Kezilahabi(1983) yeye alisema kuwa kipendi hiki kilikuwa kati ya (1885-1945) katika kipindi hiki ushairi umekubwa mabadiliko ya kiutawala na kielimu na ilikuwa ni kubadilika kwa hati za Kiarabu kuwa za Kirumi. Kwa hovyo washairi wengi nao walikubwa na mkumbo huo.
Ushairi ulishamiri baada ya uhuru kwa kuzuka mashairi mbali mbali yaliyojikita katika siasa za kujitawala baada ya kupatikana uhuru. Waandishi wa Zanzibar nao hawakuachwa nyuma bali waliandika vitabu mbali mbali vya mashairi vikiwa na dhamira kadhaa za kujitawala na za kidini pia. Mifano ya kazi za kifasihi za kishairi baada ya uhuru Zanzibar ni Utenzi wa Rasil-ghuli uliotungwa na Faqih Mgeni (1975), Fungate ya uhuru na Muhammed  S. Kh (1975), Pambazuko (1982), Kimbunga na Haji G. Haji (1995) na Malenga wapya (1997) kilichotungwa na Takiluki.
Hadithi fupi.
Hadithi fupi. Msingi wa hadithi fupi ulianzishwa kwa kiasi kikubwa na mtunzi na mhakiki maarufu wa kimarekani akijuilikana kama mwasisi wa utanzu huu. Edgar Allan Poe pamoja na mhakiki maarufu kwa jina la Brander Mathews ambae ndia inayoaminika kuwa ndie aliyetumia neno la Kingereza la “Short Story” Hadithi fupi kwa mara ya kwanza.
K. W. Wamitila (2000) akimnukuu Mbatiah na   yeye akiwanukuu akina Edger Poe kupitia kitabu cha Tales kwa kusema:-
Hadithi fupi si sura katika riwaya, tukio wala kituko ambacho kimechopolewa katika hadithi fupi au kisa kirefu bali humvutia na kumteka msomaji na kumfanya aamini kuwa ingeweza kuharibika ikiwa itakuzwa na kuwa ndefu au kama itafanywa sehemu ya kazi kubwa.
Utanzu huu umekuwa sana, hasa kiuchapishaji katika fasihi za lugha za ulaya  ukilinganishwa  na Kiswahili. Hata hivyo historia ya ukuwaji wa utanzu huu ulimwenguni inalingana na kufafanana. Wandishi wengi wa hadithi fupi walianza kuandika hadithi zao na kuzichapisha magazetini. Na hadithi yengine zilishindanishwa katika idhaa ya B.B.C na hatimae kuchapishwa katika mifululizo ya vipindi mbali mbali katika vyombo vya habari. Zanzibar ikiwa ni sehemu ya wanajamii wa Kiswahili nayo haikuwa nyuma katika miaka ya sabiini Muhamed S. A aliyeandika kitabu chake kiitwacho Kicheko cha Ushindi (1978). Katika miaka ya  themanini S. A Muhamed na kitabu chake cha Si Wazimu si Shetani, Takiluki na kitabu chao cha Hapa na Pale.
Katika kuendelea na utanzu huu wa hadithi fupi miaka ya hivi karibuni waandishi wa Zanzibar waliendelea kuandika hadithi fupi wakiwemo Mw Ali Mwalim Rashid na vitabu vyake kama vile Sungura na Mbweha, Safari ya Hamadi vyote mwaka (2004), Haji Gora Haji na kitabu cha Nahodha Chui (2004).  Hii ndio historia fupi ya hadithi fupi Zanzibar.
Tamthiliya.




Nne kwa mujibu wa Mulokozi M (1996) tamthilia au drama ni fani ya fasihi iliyokusudiwa kutendwa jukwaani kwa ajili ya hadhira fulani.
Wamitila (2004) tamthilia ni utanzu ambao hutegemea mzungumzo na uigizaji ili kuwa silisha ujumbe wake..
Haji, A. I na wenzake (1981) wao wanasema kuwa tamthilia ni utungo ulioandikwa au usioandikwa ambao unalieleza na kuliweka wazo linalotaka kuwasilishwa katika hali ya kuweza kutendeka mbele ya hadhira.
Historia ya Tamthiliya kabla ya ukoloni  Zanzibar haikuwepo ikiwa ni sehemu ya Tanzania. Kulikwa na aina yengine tu za Sanaa za maonyesho ambazo ni kinyume na tamthiliya ya hivi sasa iliyoingizwa na tamaduni ngeni. Kwa hivyo tunaweza kusema kwamba tamthiliya ilianza nchini Tanzania mnamo miaka ya 1960. Katika kipindi hiki bila ya shaka kulikuwa na tabaka mbili nazo ni tabaka tawaliwa na lile tawala. Katika kuwatawala tabaka tawaliwa watawala walianzisha shule. Shule ndio iliyokuwa silaha tosha kwa wakoloni kuwatawala wenyeji. Shule zilitumika kuonesha tamthiliya zilizobeba itikadi za kibepari. Tamthiliya za kingereza zilionyeshwa na zile za kihindi zilioneshwa pia. Tamthilia zote hizi zililenga kuimarisha tamaduni ngeni. Waafrika hawakuwa na nafasi ya kusawiri maisha yao. Mifano ya tamthilia zilizokuwepo wakti huo ni kama zile za Shakespeare kama Hamlet, Macbeth, Romeo na Juliet na nyengine nyingi.
Vichekesho ni tamthilia za mwanzo zilizoanza baada ya majilio ya wageni wananchi waliigiza vichekesho kwa kuamini kuwa ni kitendo chenye kufurahisha na kuburudisha tu.
Katika miaka ya 1957 hadi 1960 vichekesho na tamthilia fupifupi zilichezwa mashuleni hasa mwisho wa muhula au kwa mashindano baina ya madarasa au siku za sherehe maalumu za shule hizo kama (siku ya wazazi).
Tamthiliya baada ya uhuru zilikuwa hasa ni kudumisha utamaduni wa Mwafrika hap tamthilia nyingi zilitafsiriwa kwa Kiswahili kutoka Kingereza. Tamthilia hizi zilikuwa manamo miaka ya  1969-1973. Baadhi ya tafsiri hizo ni Hakimu Mwadilifu  (1973) ya Evans Brother, Julius Kaizari (1969)  J. K Nyerere na nyeinginezo. Hapa tamthiliya ilichukuwa sura mpya kwani jamii nayo ilipaswa kujitawala wenyewe ili kujiimarisha kiuchumi na kisiasa na kifikra pia. Taasisi mbali mbali zilianzishwa ili kukuza na kuimarisha utamaduni wa Mtanzania akiwemo Mzanzibari. BAKITA kwa upande wa Tanzania Bara na BAKIZA na TAKILUKI vyombo vyote hivi vilianzishwa ili kukuza na kuendeleza waandishi wanaoandika katika Kiswahili. Dhamira nyingi zilijitokeza ili kuakisi hali halisi ya wakati huo. Hapa masanii Muhamed S. A  zilipamba moto zikiwemo Kivuli Kinaishi (1990), Amezidi(1995), Kitumbua Kimeingia Mchanga (2000) na tamthilia ya Mazonge(2004) ya mwandishi Ali Mw. Rashid.

Kwa muktadha huo tumeweza kuona maendeleo ya Fasihi Andishi ya Zanzibar kabla ya majilio ya wageni vipengele(kama  Hadithi fupi, Riwaya, Ushairi, Tamthilia) vyote tulivyovijadili vilikuwa vya namna ya kienyeji vikiendana na amali za wenyeji (Wazanzibar na Watanzinia kwa ujumla ) na baada ya uhuru  ambapo vipengeli hivyo vilichota baadhiya miundo na namna ya wasilishaji wake kuendana na hali ya jamii ilivyo kisiasa, kijamii, kiuchumi na kitamaduni.   




MAREJEO
Haji, A. I na wenzake (1981) Misingi ya Nadharia ya Fasihi: Berlin Arlov Sweden.
Madumulla, J.S(2009) Riwaya ya Kiswahili, Historia ya Uchambuzi. Nairobi Sitima Printer and Stations Ltd.
Mulokozi,M.M (1996) Utangulizi wa Fasihi ya Kiswahili Dar-es-salaam, TUKI.

Nkwera F.V (1978) Sarufi na Fasihi Sekondari na Vyuo . Dar-es-salaam Tanzania Publishing House.
Massamba. D. P.B (2003)Utunzi wa Ushairi wa Kiswahili katika Makala za Semina ya Kimataifa ya Waandishi wa Kiswahili (iii) Fasihi. Taasisi ya Uchambuzi wa Kiswahili Dar-es-salaam

Wamitila K.W (2010) Kichoche cha Fasihi Simul izi na Andishi, English Press. Nairobi.  

Edwin Semzaba(OSW 208) Tamthilia ya Kiswahili. Chuo Kikuu Huria. Tanzania.  


No comments:

Post a Comment